Friday 25 April 2014

SIKU 67 ZA BUNGE LA KATIBA ZILIVYO TAWALIWA NA MIPASHO.




Dodoma. Bunge Maalumu la Katiba linaahirishwa leo baada ya kukutana kwa siku 67 bila kupitisha hata ibara moja kati ya 240 zilizomo katika Rasimu ya Katiba.
Badala yake Bunge hilo likiongozwa na Samuel Sitta “Mzee wa Kasi na Viwango” linaahirishwa hadi Agosti, mwaka huu likiendelea kujadili Sura ya Kwanza na ya Sita zenye jumla ya Ibara 19, zinazohusu masuala yanayojenga msingi wa aina ya Muungano unaopendekezwa.
Tume ya Mabadiliko ya Katiba katika rasimu iliyowasilishwa bungeni na aliyekuwa Mwenyekiti wake, Jaji Joseph Warioba ilipendekeza muundo wa shirikisho lenye serikali tatu, pendekezo ambalo limeligawa Bunge hilo vipande viwili.
Kutokana na mgawanyiko huo, kauli zenye utata, kejeli, matusi, dhihaka na ubaguzi ni mambo yaliyoshika hatamu katika mjadala wa sura hizo mbili, huku viongozi wa Bunge; Sitta na Makamu wake, Samia Suluhu Hassan wakilaumiwa kwa kushindwa kudhibiti hali hiyo.
Mwanzoni mwa wiki hii, Mjumbe wa Bunge hilo, Ezekiah Oluoch alimshutumu Sitta kwamba ameshindwa kudhibiti nidhamu katika Bunge na kwamba ndiye chanzo cha kuondoka kwa wajumbe wapatao 200 ambao ni wanachama wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
“Mwenendo wa Bunge Maalumu ulikuwa na dalili zote za kuonyesha kungetokea matatizo ndani yake kutokana na mipasho ambayo ilikuwa ikitokea kwa wajumbe pamoja na lugha ambazo siyo za staha wakati wa kutengeneza kanuni,” alisema Oluoch na kuongeza:
“Kwanza matumizi ya lugha zisizo na staha, mwenyekiti anaruhusu wajumbe kuchangia hoja kwa kupeana mipasho bila kujali hoja iliyopo mezani kinyume na kanuni,” alisema Olouch.
Hata hivyo, Suluhu alisema amekuwa akiendesha Bunge hilo kwa umakini mkubwa na kwamba kila anaposikia lugha chafu amekuwa akiwabana wajumbe kwa kuwaamuru kufuta kauli au kuomba radhi kwa matamshi. “Sipendezwi na lugha chafu, kwa hiyo mojawapo ya mambo ambayo huwa najitahidi kusikiliza kwa makini kila michango inapotolewa na wajumbe bungeni ni kubaini kama wametumia lugha zisizostahili, kisha kuchukua hatua kwa mujibu wa kanuni zetu,” alisema Suluhu.
Alikiri kwamba wapo baadhi ya wajumbe ambao wamekuwa wakigoma au kukataa kuomba radhi na kwamba masuala yao hupelekwa kwenye Kamati ya Maadili ambayo ina mamlaka ya kuchukua hatua zaidi kwa mujibu wa kanuni za Bunge hilo.
Matakwa ya Kanuni
Sehemu ya Tano ya Kanuni za Bunge Maalumu inatoa mwongozo wa mambo yanayokatazwa na yale yanayopaswa kufuatwa wakati wa mjadala.
Kanuni ya 46 imeorodhesha mambo yasiyoruhusiwa ambayo ni pamoja na kusema uongo, kutoa taarifa zisizokuwa za kweli, kuzungumza jambo lolote ambalo halipo kwenye mjadala na kutumia majina ya marais na waasisi wa Taifa kwa dhihaka.
Mwananchi

Unknown Web Developer

No comments:

Post a Comment