SARATANI YAUA WATOTO 90,000 KILA MWAKA.
Wataalamu wengi wa afya hawana uelewa wa utambuzi
wala ugunduzi wa ugonjwa huo unapomuanza mgonjwa.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dk. James Kengia
amesema watoto 90,000 hufariki kwa ugonjwa wa saratani, huku 250,000 wakiugua
ugonjwa huo kila mwaka.
Akifungua warsha ya madaktai wa vitengo mbalimbali
vikiwemo vya watoto na wanaofanya upasuaji katika Hospitali ya Rufani ya
Bugando (BMC) juzi, Dk. Kengia alisema mafunzo hayo yatawajengea uwezo wa
kutambua na kubaini dalili za kwanza za saratani kwa watoto.
Dk. Kengia alisema wahudumu wa afya wa ngazi zote
hushindwa kutambua na kugundua dalili au ugonjwa huo mapema, hivyo husababisha
watoto kufika kwenye vituo vya huduma za tiba za kansa wakiwa wamechelewa.
Alisema kwa bahati nzuri, asilimia 70 ya saratani
kwa watoto hutibika, ndiyo maana kwa nchi zilizoendelea asilimia 80 ya watoto
wenye ugonjwa huo hutibiwa na kupona kabisa.
“licha ya matokeo mazuri ya tiba ya
saratani tunayosikia kwa wenzetu, hali haipo hivyo nchini. Takwimu za Taasisi
ya Taifa ya Saratani ya Ocean Road na zile za Hospitali ya Taifa ya Muhimbili
(MNH), zinaonyesha ni kati ya asilimia 20 na 30 ya watoto wanaotibiwa na
kupona,” alisemz Dk Kengia.
Mchunguziwa Saratani, Margareth Ishengoma alisema
tatizo la saratani kwa watoto ni kubwa huambatana na changamoto nyingi, ikiwamo
ya uelewa mdogo wa wazazi, elimu duni ya saratani kwa madaktari, imani potofu,
gharama kubwa za matibabu, upungufu wa wataalamu na vituo vya ugonjwa huo.
Mkurugenzi wa shirika la kutetea watoto
walioathirika na Saratani, Walter Miya alisema watoto wanaoathirika zaidi ni
wale wanaotoka vijijini.
Miya alisema anajitahidi kuwasaidia watoto wenye
tatizo hilo kwa kutoa misaada mbalimbali ikiwamo ya fedha kwa ajili ya
kuwasafirisha kwenda hospitali.
Miongoni mwa dalili za saratani kwa watoto ni pamoja
na kuishiwa damu mara kwa mara, kuvimba sehemu ya shavu, shingo, tumbo au miguu
bila kusikia maumivu.Chanzo Gazeti la Mwananchi la Tarehe MAY 21-2015.Mnyalu
No comments:
Post a Comment